Tuesday, July 28, 2015

Adakwa na vitambulisho zaidi ya 40 vya kura


Mkazi wa Shikombe wilayani Geita, Buhula Ngassa (47) amekamatwa na vitambulisho 43 vya wapiga kura, hata hivyo amedai vilikuwa vya wateja wake waliofika kwake kusajili simu.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Geita, Joseph Konyo amesema leo kuwa mtuhumiwa Ngassa alikutwa na vitambulisho vya zamani 7 na 36 ni vipya ambavyo vitengenezwa kwa kutumia teknolojia ya BVR.
Kamanda Konyo ameongeza mtuhumiwa amejitetea kuwa vitambulisho hivyo vilikuwa ni kwa ajili ya kuwasajilia wateja waliofika kwake wakihitahitaji huduma hiyo hivyo alikuwa anaenda maeneo ya mjini ili avidurufu na kupata kumbukumbu atakazoziwasilisha kwa kampuni za simu.
Hata hivyo RPC Konyo amesema uchunguzi zaidi unaendelea kubaini ukweli wa sakata hilo. Awali, ilidaiwa kuwa mtuhumiwa alikamatwa na vitambulisho 200 vya kura lakini Jeshi la Polisi Geita limethibitisha kuwa ni 43 pekee.